MAKABURI MSIKITINI

Muhammad Faraj Salem Al Saiy

 

Kuna baadhi ya kauli zilizotolewa na baadhi ya watu kuwa Haajar na baadhi ya Mitume (‘Alayhimus Salaam) wamezikwa ndani ya Msikiti wa Makkah, na kwamba maneno hayo yameandikwa katika vitabu vya historia.

Bila shaka yoyote mwenye hoja hii anaelewa wazi kabisa kuwa waandishi wa historia hawajiwekea shuruti za usahihi wa hadithi zao, pamoja na kufanya tahakiki juu ya mlolongo wa wapokezi wa hadithi hizo (narrators), kwani wao hukusanya tu habari na kuziandika. Ama vitabu vilivyo sahihi na vinavyojiwekea shuruti za kuandika hadithi sahihi hapana hata kimoja kilichoandika juu ya jambo hilo.

Katika kitabu cha Al-Jaami’ as-Swaghiyr mwandishi wake Al-Manaar anasema;

"Hakuna hata moja katika makaburi ya Mitume yaliyo na uhakika kuwa wamezikwa hapo isipokuwa kaburi la Mtume Muhammad (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) peke yake, ama kaburi la Nabii Muusa na Ibraahiym (‘Alayhimas Salaam) ni dhanna tu, na wala hapana uhakika juu yake".

Kwa hivyo kauli hizo haziwezi kuchukuliwa kuwa ni hoja, hasa katika mambo yanayohusu itikadi za dini.

 

Ama kuhusu kauli kuwa katika kisa cha Asw-haabul Kahf, baada ya kufa kwa watu hao, palisemwa kuwa; ‘Watawajengea Msikiti’, hiyo pia si hoja, kwa sababu katika Aayah hiyo hiyo imeandikwa kuwa; wenzao walisema;

"Jengeni jengo juu yao (wasipate kupita watu kuja kuwachungulia) Mola wao Anawajua vyema (Basi inatosha)"

Wakasema wale walioshinda;

"Bila shaka sisi tutajenga Msikiti juu yao" (yaani katika pango)"

Ukichunguza utaona kuwa waliotaka wajengewe jengo, ndio waliotoa hoja ya UchaMungu kuliko hao walioshinda, na Mwenyezi Mungu hakueleza lolote katika hali zote mbili, na maneno haya ndiyo yanayokubaliwa na maulamaa wengi, wa zamani na wa sasa, akiwemo mwanachuoni wetu wa Afrika Mashariki Shaykh Abdullah Saleh Farsi (Mwenyezi Mungu Amrehemu).

 

Isitoshe, hata ikiwa tutakubali kwa ajili ya mjadala tu, basi kauli hii haileti maana yoyote ya kututaka sisi tufuate maneno yao, kwani Mwenyezi Mungu Ametuletea Mtume wetu (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) na akatufundisha yale anayotaka kutoka kwetu, na miongoni mwa aliyotufundisha ni kauli yake (Subhaanahu wa Ta’ala) katika hiyo Suratul Maidah, Sura ambayo ni ya mwisho kuteremshwa, kauli isemayo;

“Likullin ja-alna minkum shir-ataw-wa minhaaja”

"Na kila (Umma) katika nyinyi (binadamu) Tumeujaalia shari’ah yake na njia yake".

Al-Maaidah: 48

Kwa hivyo wao walikuwa na shari’ah zao na njia zao, na sisi tuna shari’ah zetu na njia zetu. Kama vile wao walivyokuwa wakiruhusiwa kumsujudia kiumbe mwenzao (Soma Surat Yuusuf) na waliharamishiwa kula baadhi ya nyama na shahamu, wakati sisi tumeruhusiwa kula vyakula hivyo na tumeharamishiwa kumsujudia yeyote mwengine asiyekuwa Mwenyezi Mungu.

 

Na kwa vile Sura hii ya Al-Maaidah inajulikana kuwa ni Surah ya mwisho kuteremshwa na kwa ajili hiyo kila kilichoandikwa ndani yake kinahesabiwa kuwa ni hukmu ya mwisho kabisa.

 

Tukirudia katika maudhui yetu ya Kaburi la Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), nilikwishanukuu hapo mwanzo kauli mbali mbali za Maulamaa zinazotofautisha hali baina ya kaburi la Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) na yale wanayozikwa watu ndani ya Misikiti au kujengewa juu yake Misikiti.

 

Ndugu zangu Waislam, hadithi sahihi ziko nyingi sana na zinaeleza kwa uwazi kabisa kuhusu maudhui yetu haya;

Kutoka kwa bibi ‘Aaishah (Radhiya Llaahu ‘anha) kuwa Ummu Habiybah na Ummu Salamah (Radhiya Llaahu ‘anha) walimhadithia juu ya kanisa waliloliona walipokuwa katika nchi ya uhabeshi, ndani yake mna picha nyingi, na bibi ‘Aaishah (Radhiya Llaahu ‘anha) akamhadithia Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), na Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akamwambia;

“Watu wale anapokuwa nao mtu mwema baina yao, basi anapokufa mtu huyo wanajenga juu ya kaburi lake msikiti (mahala pa ibada), asha wanachora juu yake picha hizo, hao ni watu wabaya kabisa kwa Mwenyezi Mungu”.

Al-Bukhaariy na Muslim

 

Hadithi nyingine;

Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) amesema;

“Ghadhabu ya Mwenyezi Mungu imekuwa kali sana juu ya watu wanaoyageuza makaburi ya Mitume yao na watu wema wao kuwa misikiti”.

Al-Bukhaariy na Muslim

 

Na akasema;

"Mola wangu usilijaalie kaburi langu likawa sanamu linaloabudiwa".

Muslim

 

Na akasema;

"Msiswali kuyaelekea makaburi wala msikae juu yake.”

Muslim

 

Na akasema

"Mwenyezi Mungu Amewalaani Mayahudi na Manaswara wamegeuza makaburi ya Mitume yao kuwa Misikiti".

Imepokelewa na Maimamu wa Sunnah wote

 

Imesimuliwa na Abdul Razak katika Musanaf yake kuwa;

"KAULI YA MWISHO KABISA ALIYOITAMKA MTUME (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) kabla ya kuirudisha roho yake iliyotwaharika kwa Mola wake aliyeiumba, alisema;

"Mwenyezi Mungu Awaangamize Mayahudi na Manaswara, wameyageuza makaburi ya Mitume yao kuwa mahali pa ibada, pasibaki na dini mbili katika bara ya Arabuni".

Hadithi hii pia imo katika Muwatwaa ya Imaam Malik

 

Kutokana na hadithi zote hizi, ndiyo maana Maulamaa wetu wakatuambia kuwa ni haramu kuswali ndani ya Misikiti iliyo na makaburi ndani yake, yote haya kwa ajili ya kuogopa laana za Mwenyezi Mungu zisije zikatusibu kama zilivyowasibu Mayahudi na Manaswara kwa ajili ya kuyageuza makaburi ya Mitume yao kuwa ni mahali pa ibada.

 

Hadithi za aina hii zilizo sahihi ziko nyingi sana, na tukiendelea kuzitaja tunaweza kujaza kurasa nyingi, isipokuwa ningependa kuongezea jambo moja, nalo ni kuwa, Imam An-Nawawiy amezielezea hadithi hizi katika kitabu cha Adhkaar katika mlango wa kutujulisha juu ya watu wanaostahiki kulaaniwa, akawataja hawa wanaotenda mambo haya kuwa ni miongoni mwa watu hao wanaostahiki kulaaniwa.

 

Kwa hivyo ni bora mtu ayakimbie mambo kama haya yenye kutatanisha na yanyomuingiza mtu katika kundi la wanaostahiki kulaaniwa na badala yake kufuata yale yaliyo dahiri na sahihi, yale yanayomkaribisha mja na radhi za Mola wake

 

Watu hawa, wanasema Maulamaa kuwa wanayajengea makaburi hayo kwa niyah njema ya kutaka kuwaigiza katika juhudi zao za kufanya ibada, lakini baada ya kupita miaka mingi wakaja vizazi wasiotambua kusudi la kujengewa, Shaytwaan ataanza kuwatia wasiwasi wake na kuwaambia kuwa wazee wao na babu zao walikuwa wakiwaabudu, kisha na wao wakawaabudu. Na hii ndiyo sababu Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akatukataza kufanya hivyo ili kuufunga mlango wa fitina tokea mwanzo wake"

Mwenyezi Mungu Anasema;

“Wamewafanya wanavyuoni wao na watawa wao kuwa ni miungu badala ya Mwenyezi Mungu, na (wamemfanya) Masihi mwana wa Maryamu (pia Mungu), hali hawakuamrishwa isipokuwa kumuabudu Mungu mmoja, hakuna anayestahiki kuabudiwa ila Yeye. Ametakasika na yale wanayomshirikisha nayo”.

At-Tawbah: 31

 

Imepokelewa kutoka kwa Imaam Ahmad na At-Tirmidhiy kuwa Uday bin Haatim At-Taaiy (Radhiya Llaahu ‘anhu) aliyekuwa mkubwa wa kabila la At-Taaiy, kwamba aliposikia juu ya kuja kwa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) na dini ya Kiislam, alikimbilia nchi ya Shaam, na hii ni kwa sababu kabila lake liliingia katika dini ya Manaswara tokea wakati wa Jahilia (kabla ya kuja kwa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam).

Katika mapambano baina ya watu wake Uday bin Haatim At-Taaiy, na majeshi ya Waislam, dada yake aitwae Savanah alikuwa miongoni mwa mateka waliotekwa na Waislam.

Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alipojua kuwa Savanah ni binti wa Haatim At-Taaiy aliyekuwa akijulikana sana na akipigiwa mifano kwa ukarimu wake, akamuacha huru. Aliporudi kwa kaka yake ambaye ni mkuu wa kabila hilo kubwa, alimshikilia sana aingie katika dini ya Kiislam.

 

Wakatoka pamoja kwenda Madiynah ili Uday amuone Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam). Alipokuwa amekaa chumbani kwa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) na msalaba wake alouvaa shingoni pake ukiwa unaning’inia kifuani pake, ikateremshwa Aaayah hiyo hapo juu;

Ittakhadhuw ahbaarahum wa ruhbaanahum arbaabam-min duuni Llaahi…”

“Wamewafanya wanavyuoni wao na watawa wao kuwa ni miungu badala ya Mwenyezi Mungu…”

Uday akasema kumwambia Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam);

Lakini hatukuwa tukiwaabudu ewe Mtume wa Mwenyezi Mungu”.

Uday masikini alikuwa akdhania kuwa ‘Ibada’ ni kumsujudia mtu au kumswalia.

Lakini Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akamsahihisha na kumfundisha nini hasa maana ya ibada, akamuuliza;

“Si (hawa wanavyuoni wao na watawa wao) walikuwa wakiharamisha yale aliyohalalisha Mwenyezi Mungu na wakihalalisha yale aliyoharamisha Mwenyezi Mungu na wao wanawafuata?”

Akasema;

Ndiyo walikuwa wakifanya hivyo”.

Mtume(Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akasema;

Basi huko ndiko kuwaabudu”.

Hapa Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) anatufundisha kuwa kuabudu, si lazima kuwe kwa kusujudu au kuswali tu, bali hata kumfuata mwenye kuhalalisha haramu na kuharamisha halali pia hiyo ni ibada.

Kisha Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akamwambia Uday (Radhiya Llaahu ‘anhu);

Ewe Uday! Unasemaje, kwani unadhurika kitu wewe panaposemwaAllaahu Akbar? Kwani unakijua chochote kingine kilichokuwa kikubwa kuliko Allaah?

Kwani unadhurika wewe panaposemwaLaa ilaaha illa Allaah’. Kwani unamjua mungu mwengine asiyekuwa Allaah?”

Kisha Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) akamuita katika Uislam na Uday (Radhiya Llaahu ‘anhu) akaitikia wito wake na akaitoa shahada ya haki.

Katika mafundisho ya Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), tutaona anatukataza kuyaabudu makaburi ya watu wema (wacha Mungu – au kama wanavyoitwa sasa Mawalii).

Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) amesema;

Ghadhabu ya Mwenyeizi Mungu imezidi kwa wale wanaogeuza makaburi ya Mitume yao na wacha Mungu wao kuwa mahala pa ibada, Mola wangu usijaalie kaburi langu likawa mahali pa ibada”.

Muslim

Na katika riwaya nyingine;

Uslijaalie kaburi langu likawa sanamu linaloabudiwa”.

Juu ya kuwa imeshapita karne nyingi tokea alipofariki Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam), inasikitisha kuona kuwa mpaka leo katika nchi nyingi za Waislam bado wapo watu wanaojishughulisha na ibada hizo za makaburi.

 

Ama kuhusu kaburi la Mtume, hali yake inakhitililafiana kabisa na maudhui haya, kwa sababu kwanza Msikiti huo haukujengwa juu ya kaburi hilo, wala Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) hakuzikwa ndani ya Msikiti, isipokuwa katika upanuzi wa Msikiti wakati wa utawala wa Banu Umayyah, kwa vile Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) alizikwa ndani ya nyumba yake iliyoambatana na Msikiti, ikabidi kaburi hilo liwe ndani yake, na Maulamaa wakafanya kila njia na kuweza kuuzungushia ukuta na kuutenga mbali na watu wanaoswali.

Hili ndilo waliloweza, pamoja na kujenga viti vya saruji mahali ambapo watu wangesimama kwa ajili ya kuswali, na kwa ajili hiyo haiwezekani mtu kusimama na kuswali hapo, na wanaweza kukaa tu na kumswalia Mtume (Swalla Llaahu ‘alayhi wa sallam) pamoja na kumuombea du’aa.